UDOM YAJIZATITI KUWA KITOVU CHA TEHAMA TANZANIA


  • 5 months
  • College of Informatics and Virtual Education

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Prof. Lughano Kusiluka, leo tarehe 10 Novemba 2023, amefanya uzinduzi wa Programu ya kuwajengea uwezo na kuendeleza ujuzi kwa wahitimu wa Shahada ya Kwanza katika masuala ya usalama wa mtandao, ambayo inaendeshwa na Benki ya Stanbic.

Akizungumza katika hafla hiyo Prof. Kusiluka, amesema kutokana na jinsi UDOM inavyofanya vizuri nchini na nje ya nchi kwenye masuala ya TEHAMA, kuna haja ya kuendeleza jitahada zaidi ili yoyote ambaye anatamani kuwa mubobezi wa masuala ya TEHAMA chaguo lake kuu liwe ni Chuo Kikuu cha Dodoma.

Aidha, Prof. Kusiluka amesema kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kipo mbioni kuanzisha kituo atamizi cha TEHAMA ( Incubation Centre) kwa ajili ya kulea, kukuza na kuendeleza vipaji vya wanafunzi wanaosoma masuala ya TEHAMA.

Naye Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri kwa Umma, Prof. Razack Lokina, ameshukuru na kuwapongeza Benki ya Stanbic kwa kuwezesha Programu hiyo na kusema kuwa Stanbic imefanya chaguo sahihi kuanzisha programu hiyo UDOM, kutokana na ubobevu waliona katika ufundishaji masuala ya usalama wa mtandao na TEHAMA kiujumla.

Akizungumzia namna Programu hiyo itakavyowanufaisha Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Mkuu wa Kitengo cha Teknolojia kutoka Benki ya Stanbic, Bw. Mussa Ally amesema kwa kuanza wataanza kwa kutoa ufadhili kwa wahitimu 10 UDOM waliofanya vizuri katika masuala ya usalama wa mtandao, kwa kuwatafutia vyuo ambavyo vitawapatia ujuzi zaidi na kuendeleza vipaji vyao kwa vitendo, sambamba na kuwapatia ajira. Programı hiyo pia itahusika kuwatafutia fursa katika makampuni mengine Ulimwenguni.
 

Comments
Send a Comment