UDOM YAIBUKA KIDEDEA MASHINDANO YA TEHAMA YA HUAWEI TANZANIA.


  • 1 week
  • The University of Dodoma

Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kimeshinda Mashindano ya Kitaifa ya TEHAMA ya HUAWEI Tanzania kwa kutoa washindi 7 kati ya 12 waliofikia hatua ya fainali. Wanafunzi hao wanatoka Ndaki ya Sayansi za Kompyuta na Elimu Angavu ( CIVE). Mashindano hayo yameratibiwa na Kampuni ya HUAWEI kutoka China, yenye lengo la kukuza na kuinua vipaji vya vijana kwenye matumizi ya Teknolojia.

Akizungumza katika hafla ya utoaji wa tuzo kwa Washindi iliyofanyika Ijumaa tarehe 10 Mei 2024 katika Ukumbi wa Maktaba UDSM; Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye, ameipongeza Kampuni ya HUAWEI kwa kuwezesha mashindano hayo na kwamba Serikali kupitia Wizara ya Habari, itaendelea kushirikiana na nchi ya China na Kampuni ya HUAWEI ili kuendelea kuwekeza zaidi kwa vijana kwa kuwa ni nguvu kazi ya Taifa. 

Aidha, amesisitiza ni muhimu kuendelea kuongeza hamasa kwa watoto wa kike kuendelea kushiriki kwa wingi katika masomo Sayansi hususani Teknolojia ya Habari (TEHAMA) kwa kuwa idadi ya Wanawake nchini wanaoshiriki katika masuala hayo ni ndogo. 

Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Mhe.Deogratius John Ndejembi, amesema kama Serikali wanaendelea kutengeneza fursa nyingi za vijana wanaofanya vizuri zaidi katika masuala ya TEHAMA, ikiwemo kuwapatia kazi za muda ili kuwajengea uwezo zaidi pindi watakapoajiriwa. 

Akizungumza katika hafla hiyo, Balozi wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian, 

amesema kutokana na mahusiano mazuri yaliyopo kati ya China na Tanzania wataendelea kutoa fursa nyingi zaidi kwa vijana ikiwemo ufadhili wa masomo na mafunzo ya muda mfupi kwa wanafunzi na wafanyakazi pamoja na kuendelea kutengeneza fursa nyingi za Ajira kwa vijana.

Naye, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Prof Lughano Kusiluka, amewapongeza wanafunzi waliofanya vizuri katika mashindano hayo na kuahidi Chuo kuendelea kuwataarisha wanafunzi vizuri vijana katika masomo yao ili washinde katika mashindano ya kimataifa. Aidha, ametoa wito kwa wanafunzi kujitokeza kwa wingi kushiriki mashindano mbalimbali kila yanapotokea ili kuendelea kuifanya UDOM kuwa ya mfano kitaifa na kimataifa. 

Amewashukuru HUAWEI kwa jitihada zao za kuibua vipaji, na kuwaomba kuwekeza katika Utafiti na kituo cha kuendelea kulea vijana wa naona Tanya vizuri hata wanapomaliza masomo yao ili kutokupoteza vipaji na ubunifu wao. 

Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi walioshinda mashindano hayo, Bi. Pulcheria Sumia kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma, amewataka watoto wa kike kutokuwa na wasiwasi na uwoga wa kushiriki mashindano yoyote kwani mbali na kushiriki zipo faida nyingi sana zinazopatikana.

Vyuo vingine vilivyoshiriki na kuibuka washindi kwenye Mashindano hayo ni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Taasisi ya Technolojia Dar Es Salaam (DIT).

Comments
Send a Comment